Mbwana Samatta alianza safari yake ya ‘Pre Season’ Julai 8 kwa kuichezea Genk kwenye mchezo wa kirafiki dhidi ya Lierse ya Ubelgiji
Licha ya kuingia akitokea benchi, nahodha huyo wa timu ya taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ alionyesha kiwango bora akiwasumbua sana walinzi Lierse
Dakika ya 84 Genk ikiwa inaongoza kwa bao moja, Samatta aliifungia timu hiyo bao la pili na kufanya iibuke na ushindi wa mabao 2-0
Baada ya mchezo huo Genk ikapumzika kwa siku tatu pekee kabla kuvaana na Willem II kutoka nchini Uholanzi, Julai 12.
Genk iliyopania kutisha msimu huu iliibamiza Willem mabao 4-0
‘Vurugu’ za Samatta ziliendelea kama kawaida
Mwisho wa siku akaifungia bao moja maridadi katika ushindi huo mnono
Hamu ya mashabiki wa Genk ilikuwa ni kuiona timu yao ikiibuka na ushindi katika mchezo wa kirafiki uliofuata dhidi ya vigogo Ajax.
Nyota huyo hakuacha kuwaonyesha kazi walinzi wa Ajax
Kuna wakati iliwalazimu kufanya madhambi ili kumpunguza kasi nyota huyo ambaye kipaji chake kilianza kuonekana kwenye timu ya mtaani kwao Mbagala jijini Dar es Salaam iitwayo Kimbangulile FC
Rafu hizo hazikumzuia Samatta kuendelea na ‘yake’
Kuna wakati mabeki wa Ajax walilazimika kumkaba wawili kwa pamoja
Lakini bado mtoto huyo wa afisa mstaafu wa jeshi la Polisi alifanikiwa kuwaacha solemba
Samatta aliifungia Genk bao moja katika sare ya mabao matatu dhidi ya Ajax
Baada ya kufunga katika mechi zote tatu za mwanzo za maandalizi ya msimu mpya wa ligi, Samatta anatarajiwa kushuka tena dimbani kesho timu yake ikipambana na Bocholt ya Ubelgiji kabla ya kumalizia kwa kuvaana na Everton Julai 22.